Ukraine: Jeshi la Urusi latishia kushambulia "vituo" vya komandi ya jeshi Kyiv
Katika siku ya 49 ya uvamizi wa Urusi nchini Ukraine, Rais wa Marekani Joe Biden ametaja vitendo vya Urusi nchini Ukraine kuwa ni "mauaji ya halaiki", akiongeza kuwa Rais wa Urusi Vladimir Putin "anajaribu kutokomeza Ukraine".
Imechapishwa:
Jeshi la Urusi linatishia kushambulia vituo vya komandi ya jeshi katika mji mkuu wa Ukraine wa Kyiv. Moscow inaishutumu Ukraine kwa rusha makombora na kufanya hujuma katika ardhi ya Urusi.
Rais wa Ukraine Zelensky ameomba tena silaha (ndege za kivita, magari ya kivita, vifaru, mfumo wa kuzuia makombora) kutoka kwa washirika wake wa Magharibi kutokana na uvamizi mkubwa wa Urusi. Kisha amejadiliana na Rais wa Marekani Joe Biden kuhusu zoezi mpya la kumpa vifaa vya kijeshi.
Kwa upande mwingine zaidi ya wanajeshi elfu moja wa Ukraine wamejisalimisha kwa vikosi vya Urusi katika mji wa Mariupol, Wizara ya Ulinzi ya Urusi imesema leo Jumatano. Siku ya Jumanne, mamlaka za kikanda kusini mashariki mwa Ukraine zilitathmini idadi ya vifo vya takriban watu 20,000 katika bandari ya kimkakati ya Bahari ya Azov iliyozingirwa kwa wiki kadhaa ambapo mapigano sasa yamejikita katika eneo kubwa la viwanda.
Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz anatarajiwa mjini Kyiv kwa "maamuzi ya kivitendo" ikiwa ni pamoja na utoaji wa silaha nzito kusaidia Ukraine katika kukabiliana na mashambulizi ya Urusi, mshauri wa rais wa Ukraine amesema leo Jumatano. Wakuu wa nchi za Poland na Baltic pia wanaenda katika mji mkuu wa Ukraine "kumuunga mkono" rais wa Ukraine "wakati wa maamuzi kwa nchi hii".