Afghanistan: Kundi la kwanza la Wafaransa kutoka Afghanistan lawasili Ufaransa
Kundi la kwanza la raia wa Ufaransa 41 waliondolewa nchini Afghanistan, waliwasili jijini Paris Jumanne jioni. Ufaransa pia inatazamia kuwarejesha raia wa Afghanistan walioshirikiana na jeshi lake nchini Afghanistan.
Imechapishwa:
Ndege ya jeshi la Ufaransa A310, yenye rangi tatu, blu-nyeupe-nyekundu, ilitua kwenye uwanja wa ndege wa Roissy-Charles-de-Gaulle mwendo wa saa 11:30 jioni, ikiwa na abiria 41 kutoka Afghanistan. Waliondoka Kabul wakati Taliban ilikuwa ikihibiti mji mkuu Kabul na maeneomengine ya nchi. Kabla ya kurudi nchini Ufaransa, ndege hiyo ilitua kwanza Abu Dhabi, katika Umoja wa Falme za Kiarabu.
Shirika la habari la AFP, likinukuu Wizara ya Mambo ya Ndani, imebainisha kuwa watu hawa 41 ambao wamewasili Ufaransa ni raia wa Ufaransa wenye asili ya "nchi washirika", lakini kwamba hakuna Waafghanistan kati yao. Chanzo cha Wizara ya majeshi kimeongeza kuwa mbali na watu hawa 41, karibu askari sitini wa Ufaransa, wanaorejea kutoka operesheni za kigeni, pia walikuwa katika ndege hiyo. Zoezi la kuhamisha watu waliopo nchini Afghanistan linaloendeshwa na Ufaransa limepewa jina la Operesheni Apagan.
Ufaransa pia inatazamia kuwarejesha raia wa Afghanistan walioshirikiana na jeshi lake nchini Afghanistan.
Awali Waziri wa Majeshi Florence Parly alisema jitihada zinafanywa kuwaondoa Wafaransa wengine waliokwama jijini Kabul.
Katika hotuba yake kwa taifa Jumatatu usiku rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alisema Afganistan, isiruhusiwe tena kuwa sehemu ya kuwapa hifadhi magaidi.