Boris Johnson ajiandaa kuwakabili wabunge wa upinzani, baada ya uamuzi wa Mahakama ya Juu
Wabunge nchini Uingereza wanarejea bungeni leo, baada ya Mahakama ya Juu Jumanne wiki hii, kuamua kuwa hatua ya Waziri Mkuu Boris Johnson kusitisha bunge kwa wiki tano, ilikuwa kinyume cha sheria.
Imechapishwa:
Waziri Mkuu Boris analazimika kuondoka mapema kwenye Mkutano Mkuu wa umoja wa Mataifa jijini New York, kuwakabili wabunge wa upinzani.
Boris hata hivyo amesema hakubaliani na uamuzi huo wa Mahakama.
Akisoma uamuzi huo, jaji mkuu wa mahakama ya juu ya Uingereza Brenda Hale, amesema majaji wa mahakama hiyo wamefikia uamuzi huo kwa pamoja, na kuongeza kuwa uamuzi wa Johnson kuahirisha bunge haukuwa halali.
“Kwa hiyo mahakama imehitimisha kwamba uamuzi wa kumshauri Malkia kusitisha shughuli za bunge ulikuwa kinyume na sheria, kwa sababu matokeo yake yalilitatiza bunge, au yalilizuia bunge kufanya majukumu yake ya kikatiba, bila sababu yoyote ya msingi, “ Rais wa mahakama hiyo hiyo, Lady Hale amesema.
Hata hivyo Boris Johnson amegoma kujiuzulu baada ya pigo hilo la mahakama ya juu.
Akizungumza kwa mara ya kwanza baada ya uamuzi huo wa mahakama mjini London, Boris Johnson ambaye yuko mjini New York akihudhuria Hadhara Kuu ya Umoja wa Mataifa, amepuuza miito iliyotolewa na wanasiasa mbali mbali wakimtaka ajiuzulu, akisema kuwa kwa maoni yake, uamuzi wa mahakama ya juu haukuwa sahihi.