Mahakama ya Ujerumani yaagiza Puigdemont kuendelea kushikiliwa
Mahakama ya Ujerumani imeagiza kuendelea kushikiliwa kwa aliyekuwa rais wa eneo la Catalonia Carles Puigdemont kusubiri uwezekano wa kurejeshwa nchini Hispania ambako anakabiliwa na mashtaka ya kufanya uasi.
Imechapishwa:
Puigdemont ataendelea kusalia kizuizini kwa wakati huu, hadi pale uamuzi utakapofanyika kuhusu mchakato wa kurejeshwa," imesema mahakama ya mkoa wa Kiel kaskazini wa Ujerumani.
Kushikiliwa kwa kiongozi huyo nchini Ujerumani kumesababisha maandamano kwenye eneo la Catalonia.
Kukamatwa kwake kumekuja miezi mitano tangu akimbie nchi yake baada ya mahakama kuu kuagiza akamatwe na kushtakiwa kwa makosa ya kufanya uasi kutokana na kura ya maoni kuamua eneo hilo kujitenga.
Mahakama hiyo ilitupilia mbali maombi ya mawakili wa Puigdemont ambao walitaka mteja wao aachiwe huru kupisha mchakato wa kesi yake kuendelea.
Puigdemont alikamatwa siku ya Jumapili punde baada ya kuvuka mpaka kuingia Ujerumani akitokea Denmark, hatua iliyotokana na waranti ya umoja wa Ulaya ya kukamatwa kwake.
Kwa mujibu wa mwanasheria wake Jaume Alonso-Cuevillasm anasema mteja wake alikuwa njiani kurejea nchini Ubelgiji ambako ndiko alikokuwa amekimbilia tnagu atoroke nchi yake.
Kuzuiliwa kwake kunaendeleza sintofahamu ya mvutano kuhusu eneo hilo kujitangazia uhuru wake na kusababisha mzozo mbaya wa kisiasa na Uhispania katika miongo kadhaa.