Bunge la Seneti la Uhispania lapiga kura kuhusu udhibiti wa taasisi za Catalonia
Bunge la Catalonia limepitisha azimio Ijumaa hii Oktoba 27 linalotangaza kuwa eneo la Catalonia linajitenga na Uhispania na kuwa taifa huru kabla ya kuimba wimbo wa uhuru huku upinzani ukisusia kikao hiki cha bunge.
Imechapishwa:
Wakati huo huo Mjini Madrid, bunge la Seneti limeidhinisha eneo la Cataloni kuwa chini ya mamlaka ya serikali kuu ya Uhispania yenye makao yake makuu mjini Madrid.
Baada ya kikao hicho cha bunge, Rais wa Catalonia Carles Puigdemont amewatolea wito wakazi wa eneo hilo kuwa watulivu na wenye amani.
Mapema alaasiri Waziri mkuu wa Uhispania Mariano Rajoy aliitisha kikao cha dharura cha Baraza la Mawaziri ambacho kimepangwa kufanyika saa 12 jioni. Hapo ndipo hatua za kwanza zitachukuliwa, yaani kufutwa kwa serikali ya CAtalonia na idara ya usalama ya Catalonia itakua chini ya mamlaka ya serikali kuu ya Uhispania. Hatua ambazo itakuwa vigumu kuzitekeleza, kwa sababu wanaharakati wa uhuru tayari wameitisha kampeni ya kutotii serikali kuu ya Uhispania.
"Kwa upande wa umoja wa Ulaya, hakuna mabadiliko, " Donald Tusk ameandika kwenye Twitter. Uhispania inabaki ni mshirika wetu. Rais wa Baraza la Ulaya ametoa wito kwa serikali ya Uhispania kuweka mbele "nguvu ya hoja, si hoja ya nguvu".
Tangu kuanza kwa mgogoro wa Cataloni, Umoja wa Ulaya umekua ukionyesha uungwaji wake mkono kwa serikali kuu ya Uhispania, kwa kuheshimisha "Katiba ya Uhispania".