NATO yasema Urusi inaendelea kuchochea machafuko nchini Ukraine
Muungano wa Majeshi ya nchi za Magharibi NATO unasema Urusi imedhirisha wazi kuwa haina nia ya dhati ya kumaliza mzozo wa Ukraine. Katibu Mkuu wa NATO Anders Fogh Rasmussen amesema Moscow inatumia mbinu mpya ya kuwapa silaha wapiganaji na kuendelea kuchochea machafuko Mashariki mwa Ukraine.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Aidha, Rasmussen ameonya kuwa Muungano huo unathathmini upya uhusiano wake na Urusi ambayo anasema imeshindwa kuheshimu maafikiano ya Kimataifa ya kusitisha machafuko Mashariki mwa Ukraine.
Haya yanajiri baada ya kuripotiwa kwa mapigano mapya kati ya wapiganaji wanaoiunga mkono serikali ya Urusi na wanajeshi wa Ukraine katika mpaka wa Urusi na Ukraine katika jimbo la Luhansk Jumanne usiku.
Mawaziri wa Mambo ya nje kutoka nchi wanachama wa NATO wanakutana jijini Brussels kuthathmini namna ya kuisaidia Ukraine kijeshi.
Matumaini kati ya wapiganaji hao na serikali ya Ukraine kutekeleza usitishwaji wa mapigano kwa kipindi cha juma moja, yamegonga mwamba baada ya ndege ya kijeshi ya Ukraine kudunguliwa na wapiganaji hao.
Rais wa Urusi Petro Poroshenko alikuwa ameahidi kuwa ikiwa hali ya utulivu itashuhudiwa Mashariki mwa nchi hiyo kufikia siku ya Ijumaa, atazungumza ana kwa ana na wapiganaji hao.
Jeshi la Ukraine linawatuhumu wapiganaji hao kuvunja mwafaka wa kusitisha mapigano mara 44, huku wapiganaji hao wakisema hakukuwa na kitu kama hicho.
Urusi kwa upande wake, imeendelea kusisitiza kuwa haiwaungi mkono wapigaji hao kwa kuwapa silaha na kutuma wanajeshi wake Mashariki mwa Ukraine.
Mataifa ya Umoja wa Ulaya na Marekani yametishia tena Urusi kuiwekea vikwazo ikiwa hali ya mapigano itaendelea.