Uchaguzi wa urais Ufaransa: François Fillon aomba radhi lakini haachii ngazi
François Fillon amejieleza Jumatatu hii, Februari 6 mchana katika mkutano na waandishi wa habari. Mgombea wa mrengo wa kulia na katikati katika uchaguzi wa urais amejieleza kwa ufafanuzi zaidi kuhusu shutuma zilizotolewa dhidi yake, ikiwa ni pamoja na ajira ya mkewe na watoto zake Bungeni.
Imechapishwa:
François Fillon kwanza amesisitiza kuhusu kazi yake ya muda mrefu katika siasa. "Kwa sasa ni miaka 32 sina hofu na vyombo vya sheria, " Bw Fillon amekumbuka.
Mgombea wa mrengo wa kulia na katikati katika uchaguzi wa urais amesema kuwa hana hatia kwa shutuma zinazotolewa wiki mbili sasa. "Nakabiliwa na mashambulizi ya vurugu yasiyokuwa ya kawaida," Bw Fillon amesema akishutumu, huku akihakikisha kwamba kupitia kashfa hizi zinazopeperushwa katika vyombo vya habari, "ni mgombea wa mrengo wa kulia na katikati anayelengwa ".
François Fillon amehakikisha kwamba mambo haya ni "sahihi na yako wazi," akitaja kazi tofauti aliyoifanya mkewe, Penelope. Ameeleza kuwa kwa miaka 15, mkewe alipokea mshahara wa wastani wa kila mwezi wa Euro 3677 pesa taslimu." Bw Fillon amebaini kwamba mshahara huyo ulitolewa kulingana na sheria kwa mtu mwenye shahada ya Sheria na Lugha. Waziri Mkuu huyo wa zamani pia ameahidi kuchapisha kwenye mtandao siku ya Jumatatu jioni "maelezo yote kuhusu mali yake."
François Fillon aomba radhi
Lakini mgombea huyo ameomba radhi kwa wananchi wa Ufaransa, na kutambua kuwa alifanya "kosa" kwa kumuajiri mkewe. "Kuna mazoea ya zamani katika siasa, mazoea ambayo hayakubaliki tena," amesema mbele ya waandishi wa habari zaidi ya 200, akimaanisha "ushirikiano wenye uaminifu ambao leo unazua tuhuma."
Kwa upande wake, anasema hakuna sababu ya kurejesha kiasi cha pesa alichopkea mkewe.