Watu wasiopungua kumi na mmoja wauawa katika vurugu nchini DRC
Machafuko yaliyozuka katika mji wa Kinshasa na katika miji kadhaa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo yamesababisha vifo vya watu zaidi ya kumi na mmoja Jumanne hii.
Imechapishwa:
Wakati huo huo kiongozi wa kihistoria wa upinzani Etienne Tshisekedi amewatolea wito wafuasi wa upinzani kuandamana kwa amani dhidi ya kubaki mamlakani kwa rais Joseph Kabila, ambaye muhula wake wa pili umemalizika Jumanne hii Desemba 20.
Kulingana na vyanzo rasmi, watu tisa waliuawa katika mji mku, Kinshasa, na mwawili katika mji wa Lubumbashi, mji wa pili kwa ukubwa. Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (MONUSCO) ulibaini muda mfupi kabla ya kuchunguza ripoti yenye kuaminika ya watu ishirini ambao inasadikiwa kuwa waliuawa katika mji mkuu wa nchi hiyo, Kinshasa na wengine kujeruhiwa katika maeneo ya Boma na Matadi. Hata hivyo idadi hiyo ya watu ishirini imefutiliwa mbali na serikali ya Congo.
"Katika mji wa Kinshasa, watu tisa waliuawa," msemaji wa serikali, Lambert Mende ameliambia shirika la habari la AFP, huku akisema kuwa miongoni mwa waliouawa kuna "waporaji sita" na "polisi mmoja" pamoja na wapita njia wawili waliouawa kwa risasi hewa.
Baaada ya kutawazwa Jumanne hii mchana, Waziri Mkuu mpya, Samy Badibanga, aliwatolea wito raia kuwa watulivu na kujizuia na vurugu na kuvitaka vikosi vya usalama kujizuia.