Olimpiki 2024: Jiji la Paris lajiandaa mwaka mmoja kabla ya michezo kuanza
Nairobi – Ni mwaka mmoja kamili, kuelekea michezo ya Olimpiki, itakayofanyika jijini Paris mwaka 2024.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Tony Estanguet, Mwenyekiti wa Kamati andalizi ya michezo hiyo katika mazungumzo na Televisheni ya France 24, amesema mpaka sasa mipango inaendelea vema.
“Napenda kuwahakikishia kuwa, maandalizi yanakamilika. Tupo kwenye hatua ya mwisho,” amesema.
Aidha, amewahikishia usalama wale wote watakaokuja kushiriki na kushuhudia michezo hiyo mikubwa katika historia ya michezo duniani.
“Tunahakikisha kuwa usalama utaimarishwa,na yatakuwa mashindano salama,” aliongeza.
Hii itakuwa ni mara ya tatu kwa Paris kuandaa michezo hiyo, baada ya kuwa mwenyeji kwa mara ya kwanza mwaka 1900 na baadaye 1924 na yanarejea baada ya miaka 100.
Wanamichezo zaidi ya 10,000 wanatarajiwa kushiriki kwenye michezo 32 katika matukio 329 ya kimichezo.
Waandalizi wanasema, sherehe ya ufunguzi tarehe 26 Julai, 2024, itafanyika katika bustani ya Jardins du Trocadéro na pembezoni mwa mto Seine katikati mwa jiji la Paris, kabla ya mashindano kuhamia katika uwanja wa Stade de France na kuendelea hadi Agosti 11.