Ndondi: Mandonga awasili nchini Kenya kupambana na Wanyonyi
Nairobi – Na Paulo Nzioki
Imechapishwa:
Bondia wa Tanzania, Karim ‘Mtu Kazi’ Mandonga amewasili nchini Kenya kwa ajili ya pambano lake la marudiano dhidi ya Daniel Wanyonyi wa Kenya. Pambano hilo linatarajiwa kufanyika katika ukumbi wa Sarit Expo Centre jijini Nairobi Julai 22.
Katika mtindo wake wa kisasa wa mchezo wa ndondi, Mandonga ameahidi kumshinda Wanyonyi huku akizindua ngumi yake mpya ya kumkabili wanyonyi akiipea jina ‘Kinguki’.
“Kama Wanyonyi alikuwa tayari kupata ngumi ya ‘Sugunyo’, ninampa pole kwa sababu nimekuja na ngumi mpya inayoitwa ‘Kinguki’ kutoka Urusi na lazima nimshinde.
"Mashabiki wa Kenya wananipenda jinsi ninavyowapenda na ninawaomba waje mapema na kwa wingi Jumamosi kunitazama," Mandonga amesema.
Boxer Karim Mandonga 'mtu kazi' arrives in the country ready to take on Daniel Wanyonyi on Saturday. pic.twitter.com/YipqPLRNII
— The Standard Digital (@StandardKenya) July 19, 2023
Bingwa wa zamani wa chama cha Ngumi Afrika (ABU) Daniel wanyonyi ameahidi kumalizana na Mandonga na kupata ukombozi wake.
"Maandalizi yamekuwa mazuri na sasa napiga msasa. Niko katika nafasi sahihi kwa pambano hilo na ninaahidi hatavuka raundi ya kwanza," Wanyonyi alisema.
Wanyonyi alishindwa na Mandonga kwa TKO katika raundi ya tano katika Kituo cha Kimataifa cha Michezo cha Kenyatta (KICC) jijini Nairobi mnamo Januari 14 katika pambano lao la kwanza.
Katika pambano lake la mwisho, Wanyonyi alimpiga Charles Kakande wa Uganda kwa TKO mnamo Machi 25 kwenye Uwanja wa Ndani wa Kasarani sawa na Mandonga ambaye pia alimshinda Lucky Yamuzi, pia wa Uganda, siku hiyo hiyo.