Tanzania kushiriki mechi ya kufuzu kwa michuano ya Olimpiki dhidi ya Botswana
Nairobi – Na Paulo Nzioki
Imechapishwa:
Timu ya soka ya wanawake nchini Tanzania (Twiga Stars) imeingia katika hatua inayofuata ya kufuzu kwa Michezo ya Olimpiki itakayofanyika Paris 2024. Twiga Stars wamefuzu baada ya uamuzi wa DR Congo kujiondoa.
Twiga Stars ilipangwa kukutana na DR Congo Julai 10 ugenini kabla ya kuikaribisha timu hiyo Julai 18 nchini Tanzania.
Hata hivyo, DR Congo iliamua kutoshindana kutokana na kile walichotaja kama sababu zisizoweza kuepukika.
Akizungumza na gazeti la the citizen la nchini Tanzania, Ofisa wa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Clifford Ndimbo amesema Tanzania sasa itamenyana na Botswana katika raundi ya pili ya mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika Oktoba mosi.
Ndimbo ameeleza kuwa Botswana ni miongoni mwa timu saba bora kutoka makala ya mwisho ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake. Nyingine ni zilikuwa Afrika Kusini, Morocco, Zambia, Nigeria, Cameroon na Tunisia.
Aidha Ndimbo ameongeza kuwa wachezaji wa Twiga Stars ambao wapo kambini wapo tayari kwa pambano hilo na hawatavunja kambi kwa kuwa bado wanakabiliwa na kibarua kingine katika michuano ya Cecafa.
Awali, Kocha Mkuu wa Twiga Stars, Bakari Shime alisema: "Tangu mwanzo, nia yangu imekuwa kuiongoza timu yangu kwenye Olimpiki ya 2024."
Kwa mujibu wa ratiba, Guinea itamenyana na Ghana huku Uganda ikimenyana na Rwanda katika pambano la Afrika Mashariki.
Burkina Faso itamenyana na Mali katika mchezo mwingine katika raundi ya kwanza.