NFF yashtushwa na hatua ya FIFA kumfungia maisha kocha Siasia
Shirikisho la soka nchini Nigeria NFF, linasema limeshtushwa na hatua ya Shirikisho la soka duniani FIFA, kumfungia maisha kocha wa zamani Samson Siasia, kutojihusisha na masuala ya soka.
Imechapishwa:
FIFA ilitangaza kuchukua hatua hiyo, baada ya kumshutumu kocha Siasia kwa kujihusisha na rushwa katika nyakati tofauti, madai ambayo ameyakanusha.
Uongozi wa NFF unasema kuwa, utahakikisha kuwa utamsaidia kocha huyo aliyeiongoza nchi hiyo katika michezo ya Olimpiki mwaka 2016 kusafisha jina lake baada ya adhabu hiyo ya FIFA.
FIFA inasema Siasia mwenye umri wa miaka 52, alishirikiana kwa karibu na Wilson Raja Perumal raia wa Singapore, anayehusishwa na upangaji wa matokeo ya mechi kadhaa za Kimataifa, kinyume na kanuni za FIFA.
Kaimu wa rais wa soka nchini Nigeria Seyi Akinwunmi amesema Siasia ambaye aliwahi kuichezea nchi hiyo mara 51, amesema tayari wamepokea ripoti ya FIFA na Mawakili wa Shirikisho, wanazipitia.