Ufaransa mabingwa wa Kombe la dunia mwaka 2018
Timu ya Taifa ya Ufaransa Les Blue imetwaa ubingwa wa fainali za kombe la dunia baada ya kusihinda Croatia mabao 4-2.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mabao ya Ufaransa yamefungwa na Paul Pogba, Kylian Mbappe, Antoine Griezman na bao la kujifunga mshambuliaji wa Croatia, Mario Mandzukic.
Mabao ya Croatia yamefungwa na Mario Mandzukic na Ivan Perisic.
Kwa ushindi huo, Ufaransa inashinda taji la pili katika historia ya Kombe la dunia, wakati Kocha Didier Deschamps pia anaweka rekodi ya kushinda taji hilo mara mbili.
Mara ya kwanza Ufaransa ilishinda taji hilo mwaka 1998, fainali zilizofanyika nchini Ufaransa, Deschamps alikuwa nahodha wa kikosi cha Ufaransa kilichoshinda taji hilo.
Hili ni mara ya kwanza kwa Croatia, taifa lenye idadi ya watu milioni 4 kufika fainali ya michuano hiyo, mara ya mwisho walifika nusu fainali mwaka 1998, fainali zilizoandaliwa na Ufaransa.
Kabla ya kufika fainali Ufaransa iliishinda Ubelgiji katika mchezo wa nusu fainali kwa bao 1-0 lililofungwa na Samuel Umtiti, Croatia wao waliwafunga Uingereza kwa mabao 2-1.
Hizi huenda zikawa fainali za mwisho za Kombe la dunia kwa wachezaji Luka Modric, Olivier Giroud ambao wana umri wa miaka zaidi ya 30.
Pia kinda wa Ufaransa, Kylian Mbappe ameweka rekodi ya kuwa mchezaji mdogo zaidi kufunga bao katika fainali za kombe la dunia, ana umri wa miaka 19.Mchezaji mwingine aliyewahi kufunga bao akiwa na umri mdogo ni Pele.
Fainali za mwaka huu, pia zilishuhudia timu za Afrika kufanya vibaya ambapo hakuna timu hata moja iliyofuzu kucheza hatua ya mwondoano.
Fainali za mwaka huu zitakumbukwa kwa uwepo wa teknolojia mpya ya usaidizi wa video, VAR.
Mbali na mfumo wa VAR, mabingwa Ufaransa walikabidhiwa kombe huku mvua kubwa ikinyesha jijini Moscow ambapo licha ya mvua kubwa rais wa Ufaransa, Urusi na Croatia bado walisalia uwanjani na kulowa wakati wakikabidhi medali na kombe.
Pia fainali hii imetazamwa na zaidi ya watu bilioni moja duniani kote.
Fainali zijazo za Kombe la dunia zitafanyika mwaka 2022 nchini Qatar,ambapo kwa mara ya kwanza zitachezwa kuanzia Novemba hadi Disemba.