Rais wa kamati ya Olimpiki nchini Italia akashifu uamuzi wa meya wa jiji la Roma
Mwenyekiti wa kamati ya Olimpiki nchini Italia, amekashifu vikali uamuzi wa meya wa mji wa Roma kukataa mji wake kuwania uenyeji wa kuandaa michezo ya Olimpiki ya mwaka 2024, ambapo ameapa kupambana.
Imechapishwa:
Huku akiuita uamuzi wa Meya kama uamuzi wa kukurupuka na kutafuta umaarufu, mwenyekiti Giovanni Malago, amesisitiza kuwa programu yao iko palepale na kwamba mpango wao ni wa kiuhalisia.
Meya Virginia Raggi aliyechaguliwa mwezi Juni mwaka huu, amesema kuwa mji wake kuandaa michezo hiyo ni kutowajibika na kutaufanya mji huo uzidi kuwa na madeni makubwa.
Tayari miji ya Boston na Hamburg imejiondoa kwenye mbio za kuwania kuwa wenyeji wa michezo hiyo ta mwaka 2024.
Malago amesema kuwa “kusikia hakuumizi”. Ila samahani sana, ilikuwa inawezekana kabisa kuandaa na kufanya vema, tutaendelea hadi pale tutakaposikia hapana ya uhakika na kupkea barua rasmi.” alisema malago ambaye alipoulizwa ikiwa kuna uwezekano wa michezo hiyo kuandaliwa Roma, alijibu “subiri tuone”.
Kauli yake imekuja saa chache kabla ya kukutana na waziri mkuu wa Italia, Matteo Renzi, ili kujaribu kumshawishi kuona ikiwa anaweza kuokoa hali inayoshuhudiwa sasa na mji wa Roma ukaendelea na kampeni ya kutafuta uungwaji mkono na baraza la mji juma lijalo.
Hata hivyo wachambuzi wa mambo wanasema kuwa, kuna uwezekano mdogo sana wa waziri mkuu Renzi kuingilia kati suala hilo.
Malago aliendelea kuuliza kuwa, ikiwa meya amekataa je ana mpango mwingine wowote wa kutengeneza ajira? Akaongeza kuwa inashangaza kuona meya anakataa wakati hakuna shirika wala taasisi ya mazingira iliyopinga wazo hilo, na kwamba hata vyama vya wafanyakazi vinaunga mkono mji huo kuomba kuandaa michezo ya Olimpiki mwaka 2024.