Nigeria yafuzu katika mzunguko wa pili licha ya kufungwa na Argentina mabao 3 kwa 2
Timu ya taifa ya soka ya Nigeria “Super Eagles” imefuzu katika hatua ya 16 bora ya michuano ya soka ya kombe la dunia inayoendelea nchini Brazil licha ya kufungwa na Argetina mabao 3 kwa 2 Jumatano usiku.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Argentina ndio iliyokuwa timu ya kwanza kupata bao kupitia mshambulizi matata Lionel Messi aliyeifungia timu yake mabao mawili katika mchuano huo.
Hadi wakati wa mapumziko, Argetina na Nigeria walikuwa nguvu sawa ya sare ya mabao 2 kwa 2 baada mshambulizi wa Nigeria Ahmed Musa kufunga bao lake la pili kwa kupiga mkwaju wa mbali.
Nigeria imekuwa nchi ya kwanza ya Afrika kufika katika hatua ya 16 bora na itamenyana na Ufaransa katika hatua ya mwondoano siku ya Jumatatu juma lijalo.
Argetina walimaliza wa kwanza katika kundi lao kwa alama 9, wakifuatwa na Nigeria kwa alama 4, huku Bosnia-Herzegovina walioifunga kwa mabao 3 kwa 1 Iran katika mchuano wake wa mwisho wakiwa wa tatu kwa alama 3.
Katika michuano mingine Jumatano usiku, Ufaransa ambayo ilimaliza kundi lake wakiwa na alama 7 baada ya kutoka sare ya kutofungana na Ecuador, huku Uswizi wakifuzu kwa kuwashinda Honduras mabao 3 kwa 0.
Uswizi ambao waliutawala mchuano huo walipata mabao yao kupitia mashambulizi matata anayeichezea klabu ya Beyern Munich ya Ujerumani Xherdan Shaqiri katika dakika ya 6, 31 na 71 ya mchuano huo.
Uswizi wao watachuana na Argetina tarehe 1 mwezi Julai kuamua ni nani atasalia katika michuano hiyo mikubwa duniani kutafuta ubingwa wa taji hilo.
Alhamisi usiku, Ghana watamenyana na Ureno, Marekani na Ujerumani.
Wawakilishi wengine wa Afrika Algeria nao watamenyana na Urusi, huku Ubelgiji wakichuana na Jamhuri ya Korea.
Ghana ambayo iko katika nafasi ya tatu na alama 1 katika kundi lao, inahitaji kushinda mchezo wa leo ili kujihakikishia nafasi ya kusonga mbele na kuomba pia Ujerumani inaifunga Marekani ambayo ina alama 4.
Ikiwa Marekani na Ujerumani zitatoka sare, Ghana au Ureno zitanduliwa nje ya michuano hiyo hata ikiwa zipata ushindi.
Algeria ambayo ni ya pili kwa kundi lao kwa alama tatu, inahitaji tu alama moja ili kufuzu na ikiwa itashinda itakuwa faraja kubwa kwa kocha Vahid Halilhodzic.
Mara ya mwisho kwa Algreia kufuzu katika hatua ya makundi iliyokuwa ni mwaka 1982, miaka 32 iliyopita ambapo walifungwa na Austria lakini timu zote mbili zikafuzu.
Urusi pia inaweza kufuzu ikiwa itaifunga Algeria sawa na Jamhuri ya Korea ikiwa inaweza kupata mabao mengi dhidi ya Ubelgiji.