Hamas yatangaza kifo cha mmoja wa makamanda wake katika shambulizi la Israel
Kundi la wanamgambo wa Kiislamu la Hamas kutoka Palestina limetangaza Jumanne, Oktoba 17, kifo cha mmoja wa makamanda wake wa kijeshi, katika shambulio anga la Israeli katikati mwa Ukanda wa Gaza, katika siku ya kumi na moja ya vita ambavyo vimesababisha vifo vya maelfu ya watu kwenye kambi zote mbili.
Imechapishwa:
Aymane Nofal, kamanda wa Brigedi za Al-Qassam, tawi lenye silaha la Hamas, aliuawa katika shambulizi la anga la "Wazayuni wahalifu" kwenye kambi ya wakimbizi ya Bureij, taarifa fupi imesema.
Jeshi la Israel halikutoa maoni yake mara moja, baada ya kuhojiwa na shirika la habari la AFP.
Wakati huo huo Jeshi la Israel limesema Wapalestina laki saba bado wako kaskazini mwa Ukanda wa Gaza, huku likiendelea kuwatuma wanajeshi wake katika eneo la mpakani kabla operesheni ya ardhini kuanza.
Onyo kutoka Iran
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema Israel haitaruhusiwa kuchukua hatua katika Ukanda wa Gaza bila matokeo - na kuonya"hatua za mapema"katika saa zijazo.
WHO yapaza sauti
Shirika la Afya Duniani WHO linasema linahitaji kuingia kwa haraka Gaza ili kutoa misaada na vifaa vya matibabu, huku likionya kuhusu janga la muda mrefu la kibinadamu.
Takriban nusu ya Wapalestina 2,800 waliouawa ni wanawake na watoto huku watu 11,000 wakijeruhiwa katika eneo la Gaza tangu kuanza kwa mashambulizi ya kulipiza kisasi ya Israel kufuatia mashambulizi mabaya ya Hamas, maafisa kutoka WHO walisema katika taarifa fupi iliyoripotiwa na shirika la habari la Reuters.