Iran na Marekani kubadilishana wafungwa
Baada ya miezi kadhaa ya kusubiri, hatimaye Tehran imetangaza kubadilishana wafungwa kati ya Iran na Marekani na kuachiliwa kwa mabilioni kadhaa ya fedha za Iran zinazoshikiliwa katika nchi kadhaa.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu mjini Tehran, Siavosh Ghazi
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema, kwa mujibu wa taarifa zake, mabadilishano ya wafungwa yatafanyika Jumatatu hii, Septemba 18.
Raia watano wenye uraia pacha Iran na Marekani wanaozuiliwa kwa miaka kadhaa kwa tuhuma za ujasusi au hatua dhidi ya usalama wa taifa wataachiliwa. Kwa upande wake, chini ya masharti ya makubaliano yaliyofikiwa kwa njia ya upatanishi huko Doha, Marekani itawaachilia Wairani watano wanaozuiliwa katika jela zao. Wawili kati yao watarejea Iran.
Fedha bilioni sita zimetolewa
Kama sehemu ya makubaliano haya, dola bilioni sita zilizozuiwa katika benki za Korea Kusini zitakabidhiwa Iran. Kadhalika, fedha za Iran zilizowekwa nchini Japani au Iraq, kwa sababu ya vikwazo vya Marekani, zitarejeshwa.
Tangazo hili linakuja wakati rais wa Iran yuko njiani kuelekea New York kushiriki katika Mkutano MKuu wa Umoja wa Mataifa. Kwa makubaliano hayo na kutolewa kwa mabilioni ya dola za fedha za Iran nje ya nchi, serikali ya rais Raisi inataka kuonyesha kwamba matarajio ya kuimarika kwa hali ya kiuchumi na kupunguzwa kwa mivutano na Marekani hivi sasa yamekaribia.