Iran: Mauzo ya mafuta yavunja rekodi licha ya vikwazo vya Marekani
Mauzo ya mafuta ya Iran yalivunja rekodi mpya mnamo mwezi Novemba na Desemba 2022. Na hii, licha ya vikwazo vya Washington dhidi ya Tehran. Miongoni mwa waagizaji wakubwa wa mafuta ya Iran ni China. Ni matunda ya ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili uliotekelezwa mwaka jana.
Imechapishwa:
Kulingana na mtaalamu wa soko la mafuta Kpler, jumla ya mauzo ya nje ya mafuta ghafi ya Iran yalifikia mapipa milioni 1.23 kwa siku mnamo mwezi Novemba 2022. Hii ina maana kwamba yamekaribia kufikia viwango vyake vya mwaka 2019.
Mshirika wa kwanza
Beijing, ambayo mara kwa mara inashutumu vikwazo vya Marekani, tayari ilikuwa mshirika mkuu wa Tehran kiuchumi na kibiashara na mteja wake mkubwa wa mafuta. Lakini kupungua kwa mahitaji ya China kwa sababu ya sera yake ya sifuri-Uviko-19 na ushindani kutoka kwa mafuta ghafi ya Urusi kwa muda, kumetishia usafirishaji wa Iran. Safari za meli za mafuta za Iran zimeanza tena.
Rekodi ya uagizaji
Miongoni mwa nchi ambako mafuta yanakoelekea, ni Venezuela, ambako Iran husafisha mafuta yake ghafi, lakini hasa China. Ili kuepuka matatizo na Washington, mafuta ghafi ya Iran yanaendelea kuingia China, rasmi kama yanatokea nchi nyingine. Kulingana na makadirio, uagizaji wa China wa mafuta ya Iran ulivunja rekodi mnamo mwezi Desemba kwa mapipa milioni 1.2 kwa siku, sawa na ongezeko la 130% kwa mwaka mmoja.