Nchi za Kiarabu zamtaka Trump kutoitambua Jerusalem kama jiji kuu la Israel
Muungano wa nchi za kiarabu umemuoya rais wa Marekani Donald Trump, kuitambua Jerusalem kuwa jiji kuu la Israel, kutasababisha vurugu katika kanda ya Mashariki ya Kati.
Imechapishwa:
Mkuu wa muungano huo Ahmed Abul Gheit ameonya kuwa iwapo rais Trump atatoa tangazo hilo, kitakuwa chanzo kikubwa cha machafuko kati ya Israel na Palestina ma hivyo kuhatarisha uwezo wowote wa mafanikio ya mazungumzo ya amani.
Muungano huo unasema kuwa Trump anataka kutoa tangazo hilo bila ya kufahamu athari zake kwa usalama wa Mashariki ya Kati na nchi za kiarabu.
Marekani kupitia mjumbe wake wa amani katika eneo la Mashariki ya Kati, Jared Kushner, amesema rais Trump anakaribia kuitambua Jerusalem kama jiji kuu la Israel.
Trump anatarajiwa kuamua baadaye leo ikiwa atatia saini sheria, itakayotoa ubalozi wa Marekani kutoka Tel Aviv kwenda jijini Jerusalem kama ishara ya kutambua kuwa ndio makao makuu ya Israel.
Palestina nayo imeendelea kuisihi Marekani kutochukua hatua hiyo ambayo inasema itaikosesha amani na jirani Israel kwa muda mrefu.
Serikali zilizopita za Marekani zilikuwa na msimamo wa kuzitaka Palestina na Israel kuamua mustakabali wa mji wa Jerusalem.