Marekani yaishtumu Syria kwa kuchoma wafungwa
Serikali ya Marekani imeishtumu serikali ya Syria kwa kuendelea na mpango wa kuua na kuchoma wafungwa gerezani, kitendo ambacho kinyume na haki za binadamu na za wafungwa.
Imechapishwa:
Marekani pia imeishtumu Syria kwa kujenga sehemu ya kuchoma maiti katika jela ya kijeshi iliyopo karibu na Damascus kwa lengo la kuficha mauaji ya kimbari ya wafungwa hasa wa kisiasa wanaoshikiliwa na serikali.
Mwanadiplomasia mwandamizi wa Marekani anayehusika na masuala ya Mashariki ya kati, Stuart Jones, amesema kwa siku wafungwa takriban hamsini wanauawa katika gereza la Sednaya.
“Syria inatekeleza mauaji hayo kutokana na kuungwa mkono na Urusi na Iran, “ amesema Stuart Jones.
Wizara ya mambo ya nje ya Marekani imeonyesha picha zilizopigwa kupitia njia ya Satelite ambazo imesema ni sehemu ya kuchoma maiti katika gereza lililopo Sednaya ambapo Umoja wa Mataifa na mashirika ya kutetea haki za binadamu yamesema maelfu ya wafungwa wameteswa na kunyongwa.
Utawala wa bashara Al Assad umekua ukilaumiwa na Marekani kwa kuendeleza mpango wa kuwakandamiza wapinzani na kujihusisha na mauaji ya wafungwa wa kisiasa pamoja na wale wanaotuhumiwa kutoiunga mkono serikali ya Damascus.