Yemen: IS yakiri kuhusika na shambulio la kujitoa mhanga Aden
Kundi la Islamic State (IS) limekiri kuhusika na shambulio la kujitoa mhanga kwa kutumia bomu lililokua limetengwa ndani ya gari.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Shambulio hilo limesababisha vifo vya watu wanane na wengine 17 kujeruhiwa Alhamisi hii kwenye kituo cha ukaguzi cha polisi, karibu na Ikulu ya rais katika mji wa Aden, mji mkuu wa pili wa Yemen.
Mshambuliaji wa kujitoa mhanga amelipua gari lake, kilometa moja na Ikulu ya Al-Maachiq, katika kata ya Crater. Vyanzo vya usalama, awali vilisema kuwa shambulio hilo lilikua limemlenga mkuu wa mkoa wa Aden, jenerali Aidarous Zoubeidi lakini kiongozi huyu ameliambia shirika la habari la Ufaransa AFP kwamba hakuwa katika eneo la tukio.
Katika taarifa iliyorushwa hewani kwenye Twitter, tawi la kundi la Islamic State (IS) katika mikoa ya Aden na Abyan (kusini mwa Yemen) limesema kuwa "shujaa aliye jitoa mhanga Abu Hanifa al-Holandi (...) amelipua gari lake lililokua limejaa mabomu katika Ikulu ya rais. "
Jina hili linaonyesha kwamba mshambuliaji ni raia wa Uholanzi.
Shambulio hili lilimegharimu maisha ya watu wanane na kuwajeruhi watu wengine 17. Askari na raia wa kawaida ni miongoni mwa watu waliojeruhiwa, Ali Saleh, mkurugenzi wa hospitali Al-Jumhuriya ambapo waathirika wamesafirishwa, ameliambia shirika la habari la Ufaransa AFP.
Wakati wa shambulio hilo, "Rais Abd Rabbo Mansour Hadi alikuwa katika ikulu, lakini yuko salama," afisa ambaye hakutaka jina lake litajwe ameliambia shirika la habari la Ufaransa AFP.