Virusi vya Corona vyaleta wasiwasi miongoni mwa wafanyibiashara nchini Kenya
Mamia ya wafanyibiashara nchini Kenya wameanza kuathirika kutokana na mlipuko wa virusi vya korona ambavyo vimeua watu zaidi ya 500 nchini China, hatua inayokuja, baada ya Shirika la ndege nchini humo kusitisha safari zake za ndege katika taifa hilo la bara Asia.
Imechapishwa:
Wengi wa wafanyibiashara wanasema wanahofia watakosa bidhaa kutoka China wakati ambao ukiwa ni msimu wa kuanza kuagiza bidhaa mbalimbali.
Katika barabara za Sheikh Karume, Duruma, Nyamakima hadi Kamukukunji, biashara zimenoga, hili ni eneo la wafanyibiashara wanaoagizia bidhaa kutoka China, bashasha zao hata hivyo zimeficha hofu kubwa inayotokana na kusambaa kwa virusi hivyo.
Anthony Mwangi ni Mwenyekiti anasema maambukizi haya yamekuka, kipindi kibaya kwa wafanyibiashara hao ambao sasa wengi huenda wakalazimika kupanga upya mipango yao ya kibiashara.
“Wachina hufungua viwanda vyao mwezi wa pili na wakenya hujiandaa wakati huo kwa hivyo tuna wasiwasi kuwa, hatutaagiza bidhaa hadi virusi hivyo vidhibitiwe," amesema Mwangi.
"Wafanyibiashara wengi walikwua mapumzikoni na sasa kwa hali hii, inaonekana tutakuwa na bidhaa chake, kwa sababu mzigo umeisha na huko China, uzalishaji umesitishwa," aliongeza.
Wanakiri sio wao tu watakaoathirika ila wakenya wengi kote nchini wanaotegemea bidhaa za China ambazo huuzwa kwa bei nafuu.
Njumwa Mwikamba mtalaam wa masuala ya uchumi anasema tishio hili linasabisha hasara kati ya nchi hizi mbili ambazo sasa zinapoteza kiasi kikubwa cha fedha kila siku kutokana na ugumu wa kupata bidhaa.
“Kenya na China zitapoteza mabilioni ya pesa na kutakuwa na upungufu katika sekta ya ajira, na tusisahau kuwa Shirika la ndege KQ limekuwa likipata hasara na huenda hali hii ikaendelea kushuhudiwa,” amesema Mwikamba
Licha ya kuwa Kenya kutothibitisha kisa chochote cha mgonjwa wa virusi vya Corona, uchumi wake huenda ukaathirika pakubwa ikiwa ugonjwa huu hautaweza kudhibitiwa kwa wakati.