Tanzania: Mchungaji maarufu wa Kanisa la Pentikoste Boniface Mwamposa ashikiliwa na polisi
Polisi nchini Tanzania wanamshikilia mchungaji wa Kanisa la Pentikoste Boniface Mwamposa kufuatia vifo vya watu 20 vilivyotokea mjini Moshi, Kaskazini mwa nchi hiyo mwishoni mwa wiki iliyopita, baada ya kukanyagana wakati wakikanyaga mafuta walioamini yalikuwa ya baraka.
Imechapishwa:
Mkuu wa wilaya ya Moshi Kippi Warioba amesema huenda idadi ya vifo ikaongezeka kutokana na wengi wa waliojeruhiwa kuwa katika hali mbaya wakiendelea kupatiwa matibabu.
George Simbachawene Waziri wa Mambo ya Ndani nchini humo amesema mchungaji huyo atawajibishwa kwa kusababisha maafa hayo.
Polisi mkoani Kilimanjaro wanasema kutokana na msongamano mkubwa wa watu waliokuwa wakitaka kukanyaga mafuta hayo, baadhi walianguka na kuanza kukanyagwa na waumini wengine ambao nao walikuwa wakijaribu kufika katika eneo ambako mafuta hayo yalikuwa yamemwagwa.
Wakati huo huo, watu wengine zaidi ya 20 wamepoteza maisha, huko Lindi kutokana na mvua kubwa zinazooendelea kunyesha katika eneo hilo.