Umri wa miaka 15 wapitishwa Tanzania kupima Ukimwi
Wabunge nchini Tanzania, wamepitisha mswada wa sheria unaoruhusu kupima maambukizi ya virusi vya ukimwi kwa vijana wenye umri wa miaka 15 bila ya idhini ya wazazi wao.
Imechapishwa:
Wizara ya afya nchini humo, inasema hatua hii itasaidia katika vita dhidi ya maambukizi ya virusi hiyo na kufikia malengo ya asilimia 90 ya watu waliambukizwa kufahamu hali zao na kutumia dawa za kupunguza makali ya virusi hivyo kufikia mwaka 2030.
Naibu Waziri wa Afya Dokta Faustine Ndugulile amesema Tanzania ni moja ya nchi ambazo zimekubali na kuridhia malengo ya dunia yanayojulikana kama 90-90-90, ikimaanisha kwamba asilimia 90 ya Watanzania wanaoishi na virisi vya ukimwi kuweza kupimwa na kutambua hali yao ya maambukizi.
Kwa mujibu wa Bw Ndugulile asilimia 40 ya maambukizi mapya ni vijana, ambapo katika asilimia hiyo 40, 80 ni wasichana.
“Changamoto imekuwa wanaume wengi hawajitokezi kupima kwa sababu ya uoga na vitu vingine, lakini takwimu pia zinaonesha kuwa maambukizi mengi mapya kwa sasa ni kwa vijana”, amebaini Naibu Waziri wa Afya wa Tanzania.
Dokta Ndugulile amesema katika hatua ya mwanzo kutakuwa na maeneo maalumu ambayo watu wataweza kununua vipimo hivyo, huku wauzaji wakiwa wamepata utaalamu na elimu ya kutosha na kwamba mnunuzi atapewa pia elimu na ushauri nasaha na utaratibu unaofuata baada ya kupima.