Polisi wakabiliana na waandamanaji jijini Kampala, wanataka "Bobi Wine" awe huru
Watu zaidi ya 70 wamekamatwa jijini Kampala nchini Uganda baada ya kutokea kwa makabiliano kati ya wafuasi wa mbunge wa upinzani Robert Kyagulanyi, maarufu kama Bobi Wine, anayeshikiliwa katika kambi ya jeshi .
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa siku ya pili jana, kulishuhudiwa maandamano katika maeneo mbalimbali ya Kampala, wakishinikiza kuachiliwa huru kwa mbunge huyo wenzake wanne.
Wanajeshi na Polisi wanaonekana wakipiga doria jijini Kampala, huku kukiwa na uwezekano mkubwa wa kuendelea kwa maandamano zaidi.
Rais Yoweri Museveni amemlaumu Kyagulanyi na wanasiasa wenzake kuchochea machafuko ya kisiasa Kaskazini mwa nchi hiyo wiki iliyopita, yaliyosababisha kukamatwa kwao.
"Kuna wale wanaodai kuwa mjukuu wangu hawezi kuongea na hali yake ya afya ni mbaya, huo ni uongo," amesema rais Museveni.
Msafara wa rais Museveni ulivamiwa na kurushiwa mawe alipokuwa amekwenda kumnadi mgombea wake wa chama tawala NRM, ambaye baadaye alishindwa katika Uchagzi huo.
Mashirika ya Kimataifa ya kutetea haki za binadamu kama Human Rights Watch na mataifa ya Magharibi yakiwasilishwa na Umoja wa Ulaya, yameshtumu namna wanasiasa wa upinzani walivyokamatwa na kupingwa.
Kyagulanyi ameshtakiwa katika Mahakama ya Kijeshi kwa kumiliki silaha kinyume cha sheria. Anatarajiwa kufika kurejea Mahakamani siku ya Alhamisi.