Mvua zinazoendelea kunyesha zaathiri maeneo mengi Kenya
Mvua kubwa inayoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya nchi ya Kenya, imesababisha kuzama kwa nyumba 30 katika Kaunti ya Makueni huku hali mbaya ya hewa ikimlazimu rais Uhuru Kenyatta kushindwa kwenda kuhudhuria kongamano la Magavana Magharibi mwa nchi hiyo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hii imesababisha mamia ya wakaazi wa Kaunti hiyo kupoteza makaazi yao huku ripoti zikisema kuwa, huenda kuna watu waliozikwa wakiwa hai baada ya kutokea kwa janga hilo.
Shirika la Msalaba mwekundu limethibitisha janga hili kutokana na mvua kubwa inayoendelea kunyesha nchini Kenya hasa katika Kaunti hiyo.
Watu katika kijiji cha Nzaui katika kaunti hiyo wamelazimika kutafuta makaazi ya muda, huku wengine wakionekana wakipanda juu ya miti kujaribu kujiokoa kutokana na maji mengi katika maeneo yao.
Katika jiji kuu la Nairobi, wakaazi wengi walishindwa kufika kazini kwa sababu ya mvua kubwa iliyonyesha usiku kucha hadi asubuhi.
Mitaa kadhaa imejaa maji, pamoja na barabara mbalimbali na kusababisha msongamano mkubwa wa magari.
Watalaam wa utabiri wa hali ya hewa nchini humo wameonya kuwa, hali hii itaendelea kwa siku kadhaa zijazo huku watu wakitakiwa kuhakikisha kuwa wapo katika eneo salama.