UNHCR: Raia elfu 60 wa Sudan Kusini waingia Sudan katika kipindi cha miezi 3
Zaidi ya raia elfu 60 kutoka Sudan Kusini wameingia nchini Sudan katika kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo ya mwaka 2017, wakikimbia njaa na vita kwenye taifa hilo changa zaidi duniani, imesema taarifa ya shirika la umoja wa Mataifa linalohusika na wakimbizi duniani UNHCR.
Imechapishwa:
Nchi ya Sudan Kusini iliundwa baada ya kutengana na majirani zaid wa Sudan ya Khartoum mwaka 2011, nchi hiyo imetangaza baa njaa kwenye baadhi ya maeneo ya nchi ambako raia wake zaidi ya laki 1 wanakabiliwa na njaa.
Awali UNHCR ilitarajia kuwa raia elfu 60 wangekuwa wameingia Sudan hadi kufikia mwishoni mwa mwaka, lakini hali imekuwa tofauti kwani idadi hiyo imefikia zaidi katika kipindi cha miezi mitatu tu ya mwanzo wa mwaka 2017.
“Idadi ya wanaowasili imevuka kiwango tulichokadiria awali, hii ikiashiria kuwa hali huenda ikawa mbaya zaidi nchini Sudan Kusini,” imesema taarifa ya UNHCR.
UNHCR inasema kuwa inatarajia kuona raia zaidi wa Sudan Kusini wakikimbia nchi yao katika kipindi cha mwaka mzima, lakini inaguswa na hali ya kupungua kwa misaada ya kibinadamu pamoja na ufadhili.
Mashirika ya misaada yamesema hali ya njaa inayishuhudiwa nchini humo imesababishwa na binadamu kutokana na vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoendelea ambapo vimesababisha maelfu ya raia kukimbia nchi yao, huku bei za vyakula zikipanda maradufu na mashirika ya misaada yakizuiwa kufika kwenye baadhi ya maeneo.
Sudan Kusini imetumbukia kwenye vita toka mwaka 2013 baada ya rais Salva Kiir kumtuhumu aliyekuwa makamu wake wa rais Riek Machar kupanga njama za kuipindua Serikali yake.
Zaidi ya raia laki 3 na elfu 65 wa Sudan Kusini, wengi wakiwa watoto na wanawake wamewasili Sudan toka mwezi Desemba mwaka 2013.