Pata taarifa kuu

Serikali ya Burundi yakataa kushiriki mazungumzo ya amani mjini Arusha

Serikali ya Burundi imesema haitashiriki katika mazungumzo ya amani yanayoanza leo kati yake na wanasiasa wa upinzani, mjini Arusha nchini Tanzania. Wakati huo huo muungano wa wanasiasa wa upinzani CNARED umekubali kushiriki katika mazungumzo hayo ambayo yanaaza Alhamisi hii hadi Jumamosi.

Rais wa Burundi Pierre Nkurunziza, ambaye serikali yake yakataa kushiriki mazungumzo ya amani ya Arusha.
Rais wa Burundi Pierre Nkurunziza, ambaye serikali yake yakataa kushiriki mazungumzo ya amani ya Arusha. REUTERS/Evrard Ngendakumana
Matangazo ya kibiashara

Msemaji wa serikali Philippe Nzobonariba amesema Bujumbura haijaridhiswa na namna mazungumzo haya yalivyoandaliwa lakini pia uwepo wa mshauri wa Umoja wa Mataifa Benomar Jamal.

Hatua hii ya serikali ya Burundi, inarudisha nyuma upatikanaji wa suluhu kuhusu mzozo wa kisiasa nchini humo hasa wakati huu ambao muungano wa vyama vya upinzani CNARED ambao viongozi wake wanaoishi nchi wakikubali kuhudhuria mazungumzo hayo, yanayoongozwa na Mratibu ambaye ni rais wa zamani wa Tanzania Benjamin Mkapa.

Rais mstaafu wa Tanzania anataka kujadiliwa kwa mara ya kwanza "masuala nyeti", kama vile muhula wa tatu wa Rais Pierre Nkurunziza unaoendelea kuzua utata na "uundwaji wa serikali ya umoja wa kitaifa," amesema mwanadiplomasia wa Afrika ambaye hakutaka jina lake litajwe.

Hata hivyo, majaribio ya kuwaleta kwenye meza moja ya mazungumzo serikali ya Burundi na upinzani walio uhamishoni hadi sasa yameshindwa. Serikali ya Bujumbura imekataa mpaka sasa kuketi kwenye meza ya mazungumzo na Cnared licha ya shinikizo na vikwazo kutoka jumuiya ya kimataifa.

"Cnared vuguvugu ambalo halitambuliwi na sheria ya Burundi na linaundwa na watu wanaotafutwa na vyombo vya sheria vya Burundi," Willy Nyamitwe, Mshari Mkuu wa mawasiliano wa rais aliliambia shirika la habari la AFP.

"Kwa hiyo ni wazi kwamba kuwaalika katika mchakato wowote wa mazungumzo ni tusi ambalo haliwezi kamwe kukubaliwa na serikali," Willy Nyamitwe alisema na kuongeza kuwa serikali ya Bujumbura inakataa kuketi kwenye meza ya mazungumzo na Cnared au mpatanishi wa Umoja wa Mataifa kwa Burundi Jamal Benomar.

Burundi imetumbukia katika mgogoro mkubwa tangu mwezi Aprili 2015 pale Rais Pierre Nkurunziza alipotangaza nia yake ya kuwania muhula wa tatu na kuchaguliwa kwa mara nyingine tena mwezi Julai mwaka huo huo. Machafuko nchini Burundi yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 500 na watu zaidi ya 300,000 kukimbilia nje ya nchi.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.