DRC: Bintou Keita azuru mashariki mwa nchi kutathmini hali ya usalama
NAIROBI – Mkuu wa tume ya umoja wa Mataifa ya kulinda amani nchini DRC, MONUSCO, Bintou Keita, anafanya ziara mashariki mwa nchi hiyo, ambapo amekutana na wadau mbalimbali wakiwemo viongozi kuangazia changamoto za usalama mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Cheza - 00:35
Kwa mujibu wa naibu msemaji wa umoja wa Mataifa, Farhan Haq, Keita ameendelea kusisitiza umuhimu wa amani na usalama, akisema tume yake iko tayari kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha usalama kwa raia.
Katika siku chache zilizopita, ameendelea kukutana na wawakilishi wa watu waliokimbia makazi yao huko Bukavu, Kivu kusini ili kujadiliana njia ya kuimarisha ushirikiano kusaidia juhudi za kupatikana usalama na amani, amesema Haq.
Hapo jana Keita akiwa huko Bunia, gavana wa mkoa wa Ituri, luteni Johny Luboya, alimweleza kuwa hali ya usalama imeimarika katika vijijini kadhaa huko Ituri kutokana na operesheni za pamoja za vikosi vya FARDC and MONUSCO.
Operesheni hii imeruhusu baadhi ya watu waliokimbia makwao kurejea haswa katika maeneo ya Tchabi na Boga katika himaya ya Irumu. Amesema luteni Luboya.
Keita amekaribisha kuzingatiwa kwa kipengele cha mahakama katika kutafuta amani, huku kwa pamoja wawili hao wakiazimia kuunganisha mafanikio haya, kwa kuimarisha njia ambazo tayari zimetumiwa hapo awali katika kukabiliana na makundi yenye silaha na kuweka mifumo mipya ya amani ya kudumu huko Ituri.