DRC: Rais Tshisekedi kuzuru China kuanzia Jumatano wiki hii
NAIROBI – Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi, anatarajiwa kuzuru China kuanzia Jumatano wiki hii hadi Jumatatu wiki ijayo, ambapo atakutana na mwenyeji wake Xi Jinping.
Imechapishwa:
Rais Tshisekedi na mwenyeji wake Xi Jinping wanatarajiwa kujadiliana na kusaini mikataba kadhaa ya biashara, ikiwa ni kufufua mikataba ya awali ambayo imekuwa haitekelezwi.
Katika ziara hiyo, ambayo imethibitishwa na Wizara ya Mambo ya nje China, inatarajiwa kufungua milango ya DRC na China kuingia kwenye mkataba wa Dola Bilioni 6 utakaowezesha wawekezaji wa Kichina kuwekeza kwenye miundo mbinu ya madini na serikali ya Kinshasa.
Tarehe 19 mwezi Mei, rais Tshisekedi aliliambia Baraza lake la Mawaziri kuwa serikali itaendelea na mazungumzo na wenzao wa China ili kupata msimamo wa pamoja kuhusu namna ya kufanikisha uwekezaji huo.
Mbali na masuala ya ushirikiano wa kiuchumi na biashara, viongozi wa mataifa hayo mawili wanatarajiwa kujadiliana kuhusu ushirikiano wa masuala ya kisiasa na usalama.
Mbali na kukutakana na rais Xi Jinping, kiongozi huyo wa DRC atakutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu Li Qiang.