Ripoti : Rwanda yajaribu kuwanyamanzisha wapinzani na wakosoaji wa serikali
Viongozi wa upinzani na wachambuzi nchini Rwanda, wanakamatwa na kufunguliwa mashataka kwa kutoa mitazamo yao ya kisiasa, kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Kimataifa la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch.
Imechapishwa:
Katika ripoti yake iliyochapishwa siku ya Jumatano, Human Rights Watch inasema, imechunguza mashtaka na maamuzi ya majaji dhidi ya raia kadhaa wa Rwanda ambao wamekuwa wakitoa maoni ya kuikosoa serikali.
Hii inaelezwa na Shirika hilo ni kwa sababu ya kuwepo kwa sheria ambazo zinaminya uhuru wa kujieleza katika taifa hilo, hasa kwa wanasiasa na wachambuzi wanaotoa maoni yao kupitia mtandao wa Youtube.
Aidha, Shirika hilo limesema limefanikiwa kuwahoji baadhi ya wanahabari waliostakiwa pamoja na wanasiasa 11 wa upinzani waliokamatwa kwa kutoa mitazamo yao.
Mkuu wa Human Rights Watch katika kanda ya Afrika ya Kati Lewis Mudge, amesema ni vigumu sana kwa watu nchini Rwanda, kutoa maoni yanayoikosoa serikali.
Ripoti ya Shirika hilo, imemnukuu mmoja wa watumiaji wa Youtube Dieudonne Niyonsenga maarufu kwa jina la Cyuma Hassan ambaye amefuguliwa mashtaka mahakamani, baada ya kuzungumzia visa vya haki za binadamu na ufisadi nchini humo na mwaka uliopita, alihukumiwa jela miaka saba.