Coronavirus : Mataifa mbalimbali yatiwa hofu na ripoti ya WHO
Mataifa 14 yameelezea hofu yao kuhusu ripoti mpya iliyotolewa na Shirika la afya Duniani WHO kuhusu chanzo cha maambukizi ya virusi vya Corona, baada ya kubainika kuwa, kuna umuhimu wa kufanya uchunguzi zaidi kubaini chanzo cha virusi hivyo.
Imechapishwa:
Mataifa hayo yakiongozwa na Marekani, yamehoji ucheleweshaji wa kutolewa kwa ripoti hiyo na kupata taarifa za kina kuhusu maambukizi hayo, huku kukiwa na madai kuwa huenda chanzo chake ni kutoka maabara mjini Wuhan nchini China.
Hata hivyo, baada ya uchunguzi wa watalaam wa Shirika la afya Duniani, wamebaini kuwa hakuna ushahidi kuwa virusi hivyo vilitoka kwenye maabara nchini China na badala yake wamesema kuwa uwezo mkubwa ni kuwa, vilitoka kutoka kwa mnyama hadi kwa binadamu.
Katika hatua nyingine, Wizara ya Mambo ya nje ya China, imeshtumu madai ya nchi hizo 14 na kusema kuwa, ripoti ya watalaam wa WHO, imeonesha kuwa Beijing, ilitoa ushirikiano wa kutoka na uwazi kuhusu utafiti wa chanzo cha virusi vya Covid 19.
Hadi sasa chanzo kamili cha virusi hivyo, bado hakijafahamika wakati huu, dunia inapoendelea kukabiliana na janga la Covid 19 ambalo limewasababisha maambukizi na maafa makubwa duniani.