Watu zaidi ya laki tano waliokufa kutokana na Corona waenziwa nchini Marekani
Rais wa Marekani Joe Biden ameagiza bendera katika majengo ya serikali kupepea nusu mlingoti kwa siku tano zijazo, kuwakumbuka watu zaidi ya laki tano ambao wamepoteza maisha kutokana na janga la corona.
Imechapishwa:
Akilihutubia taifa, rais Biden amesema idadi ya watu waliopoteza maisha nchini humo kutokana na janga la corona, imefikia karibu laki tano, na kawataka wamarekani wote kuwakumbuka wale wote waliofariki dunia na waliowapoteza wapendwa wao.
Mbali na vifo hivyo, watu wengine milioni 28.1 wameambukizwa Corona.
Rais Biden amesema inavunja moyo na amewahimiza wananchi wote nchini mwake kuvaa barakoa, kuchukua tahadhari na kutosogeleana huku akiwataka kukubali kupewa chanjo iliyokubaliwa na serikali yake.
Marekani ndio nchi yenye maambukizi makubwa na vifo vingi duniani, ambapo rais Biden amefahamisha kuwa idadi ya vifo kwenye nchi yake huenda ikapindukia 600,000.
Kabla ya kutoa hotuba yake, bendera ya taifa ilipepea nusu mlingoti katika Ikulu ya White House jijini Washington na katika majengo mengine ya serikali kote nchini pamoja na balozi zake kote duniani.
Lakini dalili pia zinaonekana kuwa hatua zimepigwa nchini Marekani na kwingineko duniani, huku idadi ya maambukizi ikipungua kwa kiasi kikubwa na utoaji wa chanjo ukiongezeka.