Joe Biden: Trump ameitumbukiza nchi hii katika hali ya sintofahamu
Joe Biden amekubali uteuzi wa chama chake cha Democratic kuwania urais mwezi Novemba mwaka huu dhidi ya rais Donald Trump wa chama cha Republican.
Imechapishwa:
Katika hotuba yake iliyoonekana kuwa na maneno ya matumaini, Biden amesema iwapo atachaguliwa, ataleta mwamko mpya na kulitoa taifa hilo kwenye giza.
Makamu huyo wa rais wa zamani, amemshtumu rais Donald Trump kwa kushindwa kutoa uongozi katika vita dhidi ya janga la Corona na hivyo, ameshindwa kuwalinda Wamarekani.
“Huu ni uchaguzi wa kubadili maisha. Hii itatupa mwanga wa namna Marekani itakavyokuwa kwa muda mrefu, “ amesema Bw. Biden
“Tunachokijua kuhusu rais huyu ni kuwa ikiwa atapatiwa miaka mingine minne, atakuwa jinsi alivyokuwa miaka minne iliyopita, “ ameongeza Joe Biden.
Aidha, ameahidi kuwa iwapo atashinda, Marekani itaendeleza urafiki wa dhati na washirka wake wa karibu lakini hatawapa nafasi viongozi Madikteta.
Joe Biden anaelekea kwenye kampeni za uchaguzi mkuu akiwa anaongoza kwa kura za maoni dhidi ya Rais Trump