Rais wa zamani wa Brazil atakiwa kutumikia kifungo chake
Nchini Brazil, Jaji Sergio Moro ametoa hati ya kukamatwa kwa rais wa zamani wa nchi hiyo Luiz Inacio Lula da Silva. Lula da Silva sasa ana saa zisizozidi 24 kuripoti kwa mamlaka husika ili kutumikia kifungo chake cha miaka 12 na mwezi mmoja kwa kosa la rushwa.
Imechapishwa:
Lula kwa sasa anakaribia milango ya jela. "Kutokana na nafasi aliyonayo kwa sasa, atakuwa na fursa ya kuripoti kwa hiari kwa polisi wa Curitiba (Kusini mwa Brazil) hadi saa 11:00 jioni (kwa saa za Brazil) Aprili 6," amesema Jaji Moro kwa mujibu wa shirika la habari la AFP.
Jaji anayehusika na kesi za rushwa nchini Brazil, Sergio Moro alimhukumu Lula mara ya kwanza mnamo mwezi Julai, hukumu iliyothibitishwa katika Mahakama ya Rufaa katikati ya mwezi wa Januari. Usiku wa Jumatano kuamkia Alhamisi, Mahakama Kuu ya Brazil ilikataa ombi la Lula da Silva ambalo lingeweza kumruhusu rais huyo wa zamani (2003-2010) kubaki huru mpaka kukamilika kwa taratibu zote za kisheria.
Taratibu kadhaa zinaendelea
Lula, mwenye umri wa miaka 72, alihukumiwa kwa kosa la kupokea ghorofa ya kifahari ilio pembezoni mwa bahari kutoka kampuni ya ujenzi baada ya kupewa zabuni.
Kiongozi huyo wa mrengo wa kushoto, ambaye pia anakabiliwa na kesi sita, amekanusha tuhuma hizo dhidi yake, akielezea ukosefu wa ushahidi na mpango wa kumzuia kuwania katika uchaguzi wa urais wa mwezi Oktoba, uchaguzi ambao anapewa nafasi kubwa ya kushinda.