Trump aapa kuibadili Obamacare licha ya kupingwa na hospitali kubwa Marekani
Viongozi wa chama cha Republican nchini Marekani wameendelea kufanya mabadiliko ya mpango wa afya wa Obamacare, licha ya kupata upinzani mkali hata kutoka ndani ya chama, hali inayoonesha kuwepo mgawanyiko mkubwa kuzunguka utawala wa Donald Trump.
Imechapishwa:
Kamati mbili za chama cha Republican walifanya mkutano Jumatano ya wiki hii, mkutano ulioshuhudia mvutano mkali kuhusu muswada ambao unatakiwa kupelekwa bungeni ili kufuta mpango wa huduma nafuu za afya uliopitishwa na rais Barack Obama.
Baada ya miaka 7 ya viongozi wa chama cha Republican kutaka kufuta mpango wa Obamacare, bado haijulikani ikiwa rais Trump atapata idadi kamili ya kura zinazohitajika kubadilisha mpango huu.
Hali hii inatokana na ukweli kuwa, hata wabunge wa Republican kwenye mabunge yote mawili wamegawanyika pakubwa kuhusu mpango mpya wa afya unataka kuchukua nafasi ya Obamacare, huku wengi wakiona ni afadhali ya mpango wa Obama.
Wabunge hao wa Republican wanasema wanataka kuuwasilisha mpango wao mpya kwenye meza ya rais kabla ya sikuu ya Pasaka mwezi wa 4.
Hata hivyo mabadiliko haya yanayotaka kufanywa na utawala wa Trump, yalipata pigo siku ya Jumatano, Machi 8, baada ya hospitali kadhaa kubwa nchini humo pamoja na taasisi za kitabibu, wakiwemo chama cha madaktari wa Marekani wanaowakilisha madaktari zaidi ya laki 2 mbili nchini humo, wameungana kupinga mabadiliko haya yanayotaka kufanywa na Serikali.
Makundi haya yameeleza hofu yao kupitias mpango mpya wa Serikali, wakisema wananchi masikini nchini humo watakosa bima ya kupata matibabu.