Washington yaituhumu Moscow kuchochea machafuko Syria
Jumatano wiki hii, Marekani imeituhumu Urusi kuchochea machafuko nchini Syria kwa kuendesha mashambulizi yanayowaua raia, na hivyo kusababisha ongezeko la wakimbizi na kuimarisha utawala mjini Damascus badala ya kudhoofisha wapiganaji wa kundi la Islamic State (IS).
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwenye uwanja wa mapambano, majeshi ya Syria yameondoa vizuizi viliyowekwa kwa muda wa wiki mbili na kundi la Isamic State katika maeneo yalio chini ya udhibiti wao katika jimbo la Aleppo (kaskazini), na kufungua upya barabara muhimu inayounganisha maeneo hayo na maeneo mengine ya Syria, kwa mujibu wa runinga ya serikali na shirika lisilo la kiserikali.
Wakiunga mkono Marekani kuisoa Moscow, mshirika wa karibu wa Bashar al-Assad, wanadiplomasia wawili, mbele ya baraza la wawakilishi la Congress la Marekani, walionyesha hatua kwa hatua jinsi Urusi ilianza kuingilia kijeshi Syria tangu Septemba 30.
Naibu Waziri wa mambo ya nje anaye husika na masuala ya Mashariki ya Kati Anne Patterson amesema kuwa Moscow inaendelea kuchochea "hali hatari ambayo tayari iko katika utata."
Tangu kuanza mashambulizi ya Urusi, takribani raia 120,000 kutoka Syria wameyahama makazi yao, ikiwa ni moja ya athari ya mashambulizi ya jeshi la Bashar Al Assad yakiungwa mkono na jesi la Urusi katika miji ya Hama, Aleppo, na Idleb, Bi Patterson ametuhumu mbele ya Kamati ya mambo ya nje ya Baraza la wawakilishi la Marekani.