Syria: mazungumzo ya Vienna ni kipima joto cha uaminifu kwa Iran na Urusi
Mazungumzo juu ya Syria yaliyopangwa kufanyika Alhamisi hii mjini Vienna ni kipima joto cha "uaminifu" kwa Iran na Urusi, washirika wakuu wa utawala wa Bashar al-Assad, katika upatikanaji wa suluhu ya mgogoro unaoendelea nchini humo, Waziri wa mambo ya nje wa Saudi Arabia amebaini.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Iran, mshirika mkuu wa serikali ya Syria, itashiriki kwa mara ya kwanza katika mazungumzo ya kimataifa juu ya mgogoro wa Syria, katika njia ya kidiplomasia iliyopendekezwa na Moscow.
Iran yenye wakazi wengi kutoka jamii ya Washia na Saudi Arabia yenye wakazi wengi kutoka jamii ya Wasuni - mataifa mawili adui yenye nguvu katika Ukanda huo wa Mashariki ya Kati, hayaelewani kianagaubaga kuhusu Syria. Tehran inatoa msaada wa kifedha na kijeshi kwa serikali ya Damascus huku Saudi Arabia ikisaidia waasi na kushiriki katika mashambulizi ya anga ya muungano wa kimataifa unaongozwa na Marekani dhidi ya kundi la Islamic State (IS).
" Kama ni wakweli, tutajua. Kama si wakweli, pia tutajua na tutaacha kupoteza muda pamoja nao ", Waziri wa mambo ya nje wa Saudi Arabia, Adel al-Jubeir, amesema wakati wa mkutano na waandishi wa habari akiwa na mwenzake wa Uingereza Philip Hammond, ambaye yuko ziarani Riyadh..
Mazungumzo ya mjini Vienna yatakuwa kipima joto kwa " nia ya Syria na Urusi ", ameongeza Jubeir, huku akibaini kwamba mazungumzo hayo yatatoa fursa ya "kuziba pengo" kati ya Iran na Urusi kwa upande mmoja, na nchi nyingine kwa upande mwingine kuhusu jukumu la Bashar al-Assad katika mchakato wa kisiasa.
" Ni lazima kuwa na uhakika kwamba Bashar al-Assad ataondoka ", Waziri wa mambo ya nje wa Saudi Arabia ameongeza.