Urusi yataka serikali ya Syria kukutana na upinzani
Wajumbe wa serikali ya Syria na wawakilishi wa makundi ya upinzani wanaweza kukutana mjini Moscow wiki ijayo, Naibu Waziri wa mambo ya nje wa Urusi, Mikhail Bogdanov, ametangaza.
Imechapishwa: Imehaririwa:
" Wiki ijayo, tunawakaribisha wawakilishi wa upinzani kwa mashauriano mjini Moscow", Mikhail Bogdanov amesema, kulingana na Interfax.
" Mkutano (...) wawakilishi wa serikali labda watashiriki katika mkutano huo ", Naibu Waziri ameongeza.
Mikhail Bogdanov hakutaja majina ya wajumbe wa upinzani ambao wangeweza kushiriki mkutano huo.
Moscow, baada ya kufutilia mbali katika hatua ya mwanzo makundi ya upinzani nchini Syria yanayopigana dhidi ya Rais Bashar al-Assad, mshirika wake mkuu katika Ukanda huo, hatimaye imejikita sana katika jitihada zake za kutatua machafuko yaliosababisha vifo vya watu 250,000 na mamia kwa maelfu ya wakimbizi pamoja na wakimbizi wa ndani.
Waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov ana mpango wa kukutana na mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kwa Syria, Staffan de Mistura, jijini Moscow Jumatano wiki hii, msemaji wa wizara ya mambo ya nje, Maria Zakharova ametangaza, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Urusi.
" Mada kuu ni mchakato wa kisiasa nchini Syria, mwanzoni wa mazungumzo halisi kati ya Damascus na upinzani ", msemaji wa wizara ya mambo ya nje wa Urusi amesema, kwa mujibu wa shirika la habari la Tass.
Katika mkutano juu ya amani nchini Syria, ambao ulifanyika katika mji mkuu wa Austria, Vienna, siku ya Ijumaa, Urusi ilitangaza kuwa ilitaka makundi ya upinzani nchini Syria kushiriki katika majadiliano juu ya mgogoro wa Syria na ilibadilishana orodha ya majina 38 na Saudi Arabia.