Coronavirus: Idadi ya vifo yazidi 2000 China Bara
Abiria waliokuwa wamekwama katika meli iliyokuwa imetengwa kwa hofu ya kuwa na abiria walioambukizwa virusi vya ugonjwa unaofahamika sasa kama Covid-19, na kuzuiwa katika bandari ya Yokohama nchini Japan, kwa muda wa siku 14, wameanza kuondoka ndani ya meli hiyo.
Imechapishwa:
Baada ya kuondoka ndani ya meli hiyo, abiria wamekuwa wakielezea namna ilivyokuwa ngumu kwao kusalia ndani ya meli hiyo kwa siku 14, baada ya kuripotiwa kuwa abiria 542 walikuwa wameambukizwa virusi hiyo.
Hatua ya kuwaruhusu abiria hawa, imekuja, baada ya kufanyiwa vipimo na kubainika kuwa walikuwa hawajaambukizwa, huku wale walioambukizwa wakiendelea kutengwa kwa muda zaidi kwa siku kadhaa kwa sababu za kiafya.
Katika hatua nyingine, maafisa nchini China wanasema idadi ya watu walipoteza maisha kutoka na maambukizi hayo, imefikia 2,004 huku wengine zaidi ya 74,000 wakiwa wameambukizwa.
Hong Kong nayo imesema mtu wa pili aliyekuwa ameambukizwa, amefariki dunia.
Mataifa mengine ambayo yameripoti vifo kutokana na virusi hivi ni pamoja na Ufaransa, Japan, Ufilipino na Taiwan.