Shirika la Afya Duniani laelezea wasiwasi wake kuhusu virusi vya Corona
Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Tedros Adhanom Ghebreyesus' ameonya kuwa maambukizi ya virusi vya Corona kwa watu ambao hawajasafiri kwenda nchini China, inazua wasiwasi mkubwa kuhusu namna ya kudhibiti maambukizi hayo.
Imechapishwa:
Kauli hii ya Mkuu huyo wa WHO imekuja, wakati huu watalaam wa Shirika hilo wakielekea nchini China kwenda kushirikiana na maafisa wa afya nchini humo kusaidia kudhibiti maambukizi zaidi.
Kufikia siku ya Jumatatu, idadi ya watu waliopoteza maisha kutokana na virusi hivi, imefikiia zaidi ya 900, huku watu wengine zaidi ya 40,000 wakiwa wameambukizwa nchini China.
Licha ya kuonekana kwa jitihada kubwa za kudhibiti maambukizi haya nchini China, WHO inaonya kuwa iwapo maambukizi haya yataendelea kusambaa kwa watu ambao hawajaenda nchini China, basi itakuwa ni hatari zaidi.
Mataifa mbalimbali hasa yale ya Maghariibi yameendelea kuwaondoa raia wake nchini China, lakini mataifa ya Afrika yamesita kufanya hivyo, kutokana na mfumo mbaya wa afya katika nchini zao kwa hofu kuwa hatua hiyo inaweza kusababisha maambukuzi zaidi.