DRC: M23 yarusha mabomu kadhaa na kuua raia watatu
Hali bado ni ya wasiwasi na tete Jumamosi hii Machi 2 katika eneo la Sake katika mkoa wa Kivu Kaskazini, Mashariki mwa DRC ambapo waasi wa M23, ambao wanakalia karibu vilima vyote vinavyoutazama mji huo, walirusha mabomu 5 siku ya Ijumaa mchana, na kusababisha vifo vya raia watatu.
Imechapishwa:
Ilikuwa ni muda mfupi kabla ya kuwasili kwa wakuu wa vikosi vya ulinzi vya Tanzania, Malawi, Afrika Kusini na Burundi huko Mubambiro.
Majenerali walioko Goma kwa sasa walienda kutembelea wanajeshi waliotumwa kama sehemu ya ujumbe wa SADC, SAMI-DRC.
Kulingana na Radio Okapi ilikuwa karibu saa 9 alaasiri kwa saa za huko, siku ya Ijumaa, ambapo mabomu 5 yaliyorushwa na waasi wa M23, kutoka kilima cha Kihuli, yalianguka kwenye kijiji cha Mubambiro, kwenye lango la mashariki la mji wa Sake.
Vyanzo vya ndani vikinukuliwa na radio Okapi vinataja vifo 3 kati ya raia, pamoja na mtoto, na baadhi ya nyumba kuharibiwa.
Kwa mujibu wa msemaji wa jeshi la FARDC, Jenerali Sylvain Ekenge, mashambulizi haya ya mabomu hayakatishi tamaa azma ya jeshi la Kongo na wakuu wa maafisa wakuu wa nchi zinazochangia ujumbe wa SAMI-DRC, wanaozuru eneo hilo.
"Magaidi walijaribu kuwazuia, kwa kurusha mabomu, lakini hawakushinda dhamira ya viongozi wa vikosi vya ulinzi waliofika Mubambiro na kuweka mikakati ya kukomesha harakati za magaidi hawa wa RDF/M23," amesema Jenerali Ekenge.
Ijumaa hiyo hiyo, risasi kadhaa zilisikika katika vijiji vilivyo karibu na Sake; na hata katika eneo la kichifu la Bwito, ambapo ndege isiyo na rubani ya FARDC ilipigwa risasi na waasi karibu na Murimbi, katika eneo la Tongo, vyanzo katika eneo hilo vinaripoti.