CAR: Takriban watu 22 wauawa katika shambulio katika kijiji cha Nzakoundou
Shambulio la watu webye silaha limelenga kijiji cha Nzakoundou katika kitongoji cha Ngaoundaye kaskazini-magharibi mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati siku ya Alhamisi, Desemba 21. Takriban watu 22, ikiwa ni pamoja na askari, waliuawa katika shambulio hili, ikiwa ni pamoja na nyumba kadhaa kuchomwa moto. Pia watu wengi walijeruhiwa.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu huko Bangui, Rolf Steve Domia-Leu
Ilikuwa asubuhi ya Alhamisi, Desemba 21 ambapo kijiji cha Nzakoundou kilikumbwa na shambulio kali la watu wenye silaha. Takriban watu 22 akiwemo mwanajeshi mmoja walipoteza maisha. Watu kadhaa waliojeruhiwa vibaya walipelekwa katika maeneo jirani, kulingana na Ernest Bonang Mbunge wa Ngaoundaye, mji ulioko kilomita 35 kutoka Nzakoundou.
Kulingana na baadhi ya vyanzo, shambulio hili lilifanywa na kundi la 3R, linaloundwa zaidi na wafugaji, dhidi ya ngome ya vikosi vya jeshi la Jamhuri ya Afrika ya Kati kulipiza kisasi kwa wizi wa mifugo ya wafugaji kwa kitendo kinachodaiwa na kundi hilo kuwa kilitekelezwa na wanajeshi wa jeshi la taifa. Washambuliaji waliondoka baada ya kuteka kijiji kizima. Idadi hiyo inaweza kuongezeka kwani watu kadhaa hawajulikani walipo.
Shambulizi hili lilizua wimbi la hasira nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati. Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyochapishwa Ijumaa hii, Desemba 22, chama cha siasa cha upinzani URCA kinatoa wito kwa mamlaka kutoa huduma ya matibabu kwa watu waliojeruhiwa, kulipa fidia kwa familia za wahanga na kujenga upya kijiji hiki. Kwa upande wake, serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati inalaani shambulizi hili na kutangaza kufunguliwa kwa uchunguzi.