Mzozo nchini Sudan: Mazungumzo ya Jeddah yasitishwa, mapigano yashika kasi
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani anayeshughulikia Masuala ya Afrika, Molly Phee, alithibitisha Juni 22, 2023 kwamba mazungumzo yaliyoandaliwa nchini Saudi Arabia kati ya wapiganaji katika mzozo wa Sudan "yameahirishwa" kwa kukosa matokeo. Nchini Sudan, mapigano kati ya jeshi na wanamgambo yameongezeka.
Imechapishwa:
Nchini Sudan, vita kati ya jeshi na Vikosi vya Msaada wa Haraka (RSF) vimeongezeka katika siku za hivi karibuni. Vita mpya, huko Kordofan Kusini, inaonekana kuzuka, kulingana na shuhuda kutoka jimbo hili la mpakani la Darfur na Sudan Kusini, tangu kumalizika kwa usitishaji vita wa saa 72 mnamo Juni 21.
Mazungumzo ya Jeddah, mji wa Saudia ambako makubaliano haya yalifikiwa, yamesitishwa rasmi na Marekani na Saudi Arabia. Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani anayeshughulikia Masuala ya Afrika, Molly Phee, alithibitisha hilo mnamo Juni 22, 2023, mbele ya Baraza la Wawakilishi.
Rasmi, kwa lugha ya kidiplomasia, alieleza kwamba majadiliano katika Jeddah "yameahirishwa" kuanzia Jumatano, kwa sababu "muundo" wa mazungumzo haukuruhusu "kupata mafanikio" yanayotarajiwa na wapatanishi.
Alitoa wito kwa serikali nyingine kuungana na Washington katika kuamua juu ya vikwazo dhidi ya wapiganaji, akiongeza kwamba Uingereza ilikuwa inazingatia kufanya hivyo, lakini kwamba Umoja wa Ulaya kwa upande wake umekuwa "ukifanya jambo hilo kwa mwendo wa kinyonga".
Sudan: Mapigano makali mjini Khartoum baada ya kumalizika kwa muda wa kusitishwa vita
Wakati huo huo, katika mji mkuu wa Khartoum, mashambulizi ya anga ya jeshi yamejibu mashambulizi ya vikosi vya FSR kwa siku mbili. Mapigano ya ardhini pia yameripotiwa, huko Omdurman na kusini mwa jiji.
Katika mikoa tofauti ya Darfur, mashambulizi makali pia yameripotiwa na kamati za upinzani za ndani. Hali ni ya wasiwasi huko El Fasher, kaskazini mwa nchi, mji ambao unawapa hifadhi ya ukimbizi mamia ya maelfu ya watu waliokimbia makazi yao.