Tunisia: Rached Ghannouchi, kiongozi wa chama cha upinzani cha Ennahda, akamatwa
Aliyekuwa spika wa Bunge la Tunisia, Rached Ghannouchi, kiongozi wa chama cha Kiislamu cha Ennahdha, amekuwa kwenye orodha ya watu wanatafutwa na mamlaka kwa miezi kadhaa. Alikamatwa jioni ya Jumatatu Aprili 17 nyumbani kwake.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu mjini Tunis, Amira Souilem
Rached Ghannouchi alikamatwa nyumbani kwake, katika mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhan siku ya Jumatatu jioni. Nyumba yake ilifanyiwa msako na kiongozi huyo wa kisiasa alipelekwa moja kwa moja kwenye makao makuu ya kikosi cha Walinzi wa Kitaifa cha kupambana na ugaidi bila hata hivyo kufahamishwa mashitaka yanayomkabili, kulingana na toleo lililotolewa na chama chake. Kwa hivyo hii inaibua 'utekaji nyara' na sio kukamatwa. Katika taarifa kwa vyombo vya habari, chama hicho kinatoa wito wa 'kuachiliwa kwake mara moja'.
Katika miezi ya hivi karibuni, kiongozi huyo wa kisiasa aliitwa mara kadhaa na mahakama zilizomshuku kuhusishwa na kesi za ugaidi, utakatishaji fedha au hata majaribio ya kuyumbisha utawala uliopo. Alijitokeza mwezi Februari katika kituo cha mahakama cha kukabiliana na ugaidi kufuatia malalamiko yanayoshutumu kwa kuwaita polisi "wadhalimu". Mpinzani huyo pia alisikilizwa mnamo mwezi Novemba 2022 na jaji kutoka kituo cha mahakama cha kukabiliana na ugaidi kwa kesi inayohusiana na madai ya kutumwa kwa wanajihadi nchini Syria na Iraq. Mnamo mwezi Julai mwaka huo huo, alihojiwa pia kwa tuhuma za ufisadi na utakatishaji wa fedha unaohusishwa na uhamishaji wa pesa kutoka ng'ambo hadi shirika la kihisani linaloshirikiana na Ennahdha.
Wapinzani zaidi ya ishirini wakamatwa
Akiwa na umri wa miaka 81, Rached Ghannouchi, spika wa zamani wa Bunge la Tunisia kabla halijazuiliwa na Rais Kaïs Saïed, naye anakumbwa na hatima kama ya wapinzani ishirini waliokamatwa tangu Februari mwaka jana. Kukamatwa huku, ikiwa ni pamoja na mawaziri wa zamani, wafanyabiashara na mmiliki Redio Mosaïque FM, kumelaaniwa na mashirika yasiyo ya kiserikali ya ndani na kimataifa.
Rached Ghannouchi alikamatwa katikati ya usiku unaoitwa "usiku wa cheo (usiku waheshima) Lailatu Al-Qadr", usiku mtukufu zaidi katika mwezi wa Ramadhani. Muda ambao umeamsha hasira ya baadhi ya wanachama wa chama cha Kiislamu cha Ennahdha, ambao wanaona kukamatwa kwa njia hii, kwa upande wa utawala, ni laana, wakati nchi hii inapitia mgogoro mkubwa wa kiuchumi.
(Pamoja na AFP)