Maelfu ya watu wayatoroka makazi yao kufuatia machafuko Kaskazini mwa Sudan Kusini
Mashirika ya Umoja wa Mataifa, yanasema machafuko yanayoendelea Kaskazini mwa nchi ya Sudan Kusini, yamesababisha maelfu ya watu kuyakimbia makwao, katika wiki kadhaa zilizopita.
Imechapishwa:
Jimbo lililoathirika zaidi ni lile la Upper Nile, na ripoti zinasema, baadhi ya watu waliyoyakimbia makwao, wamelazimika kujificha kwenye maeneo yenye madimbwi ya maji na misitu.
Tume ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia misaada ya kibinadamu OCHA, inasema machafuko hayo yamesababisha watu 9,100, kuyakimbia makwao tangu katikati ya mwezi Novemba.
Hata hivyo, tangu mwezi Agosti, Tume ya Umoja wa Mataifa, inayoshughulikia wakimbizi kusema kuwa, watu zaidia ya Elfu 20 wameyakimbia makwao, huku wengine zaidi ya elfu tatu wakikimbilia nchini Sudan.
Katika hatua nyingine, inahofiwa kuwa idadi ya watu wasiofahamika, wamepoteza maisha, wengine wametekwa huku wasichana na wanawake, wakibakwa.
Tume ya Umoja wa Mataifa, nchini Sudan Kusini imeitaka serikali jijini Juba kusaidia kusitisha mapigano katika jimbo hilo la Upper Nile.