Ghana yakumbwa na maandamano dhidi ya serikali kufuatia mdororo wa kiuchumi
Maelfu ya watu wameandamana jijini Accra nchini Ghana, kuishtumu serikali ya rais Nana Akufo-Addo, kushindwa kutatua changamoto mbali mbali hasa za kiuchumi zinazoikabili nchi hiyo.
Imechapishwa:
Kwa miezi kadhaa sasa, kumekuwa na vuguvugu la vijana ambalo limekuwa likitumia mitandoa ya kijamii kushinikiza mabadiliko nchini humo na kuikosoa serikali.
Waandamanaji wengi wakiwa vijana, wanalalamikia ukosefu wa ajira na hali ngumu ya uchumi katika taifa hilo la Afrika Magharibi.
Wakiwa wamevalia sare nyekundu na nyeusi, waandamanaji hao wamesikika wakiimba nyimbo za kizalendo na kuonesha mabango yanayoonesha changamoto wanazopitia.
Mwezi Julai kulikuwa na maandamano kama haya yaliyoandaliwa na chama kikuu cha upinzani cha NDC.
Rais Nana Akufo-Addo ambaye alichaguliwa tena kwa muhula wa pili mwezi Desemba mwaka uliopita, serikali yake imekabiliwa na deni kubwa kutoka nje, janga la Covid-19 na ongezeko la kodi ambalo limesababisha gharama ya maisha kupanda hasa ongezeko la bei ya mafuta.