Chad: Upinzani waitisha maandamano, jeshi lakataa mazungumzo na waasi
Chad inatarajia kukabiliwa na maandamano makubwa wiki hii, baada ya upinzani na mashirika ya kiraia kuitisha maandamano Jumanne wiki hii, kupinga kile wanachokiita mapinduzi ya kijeshi.
Imechapishwa:
Maombolezo ya kitaifa bado yanaendelea katika mji mkuu wa Chad, Ndjamena, lakini mashirika ya kiraia yanataka kushinikiza Baraza la kijeshi la Mpito kugawana madaraka katika kipindi hiki cha mpito.
Wakati huo huo Baraza la kijeshi linalongoza nchi ya Chad kwa kipindi cha mpito limesema halitaingia kwenye mazungumzo na waasi wanaojiita FACT waliokabiliana na wanajeshi wa nchi hiyo wiki moja iliyopita Kaskazini mwa nchi hiyo na kusababisha kifo cha aliyekuwa rais Idriss Deby.
Msemaji wa Baraza hilo la Jeshi Azem Bermandoa Agouna, ametoa kauli hiyo huku akiiomba nchi ya Niger, kusaidia kumkamata kiongozi wa kundi hilo la waasi.
Jumamosi iliyopita, waasi hao walisema wanajiandaa kusitisha mapigano, lakini jeshi nchini Chad linasema lipo kwenye vita na kundi hilo na litaendeleza mashambulizi.