Mazishi ya kitaifa ya Rais wa Chad Idriss Déby kufanyika Ijumaa
Sherehe za kitaifa za kumuaga Rais wa Chad Idriss Déby Itno, aliyeuawa Jumatatu Aprili 19 wakati akiongoza mapigano ya jeshi lake dhidi ya waasi, zitafanyika Ijumaa Aprili 23 huko Ndjamena kabla ya mazishi yake katika mkoa wake wa asili Mashariki ya mwa nchi, ofisi ya rais imetangaza leo Jumanne, Aprili 20.
Imechapishwa:
"Mazishi rasmi ya Marshal wa Chad, Rais wa Jamhuri [...] Idriss Déby Itno, aliyefariki dunia Aprili 19, yatafanyika kwenye eneo la Place de la Nation Ijumaa Aprili 23", mbele ya "marais na viongozi wa serikali wa nchi rafiki ”, kulingana na taarifa ya kiitifaki kutoka ofisi ya rais.
Jeshi la Chad limetangaza kuvunjwa kwa serikali na bunge kufuatia kifo cha rais Idriss Deby wa nchi hiyo lakini limeahidi kutakuwa na uchaguzi huru wa kidemokrasia baada ya kipindi cha mpito cha miezi 18.
Jeshi limesema Baraza la Mpito tayari limeundwa na litaiongoza nchi hiyo kwa muda wa miezi 18 kabla ya kuitishwa uchaguzi mkuu. Baraza hilo linaongozwa na mtoto wa hayati rais Deby aitwaye Mahammat na jeshi limewatolea wito raia wa Chad kuimarisha amani, uthabiti na utii wa sheria katika kipindi chote cha msiba wa taifa.