Idriss Deby, kiongozi mwenye historia ndefu ya vita dhidi ya wanajihadi
Kuuawa kwa Idriss Deby Itno kiongozi wa muda mrefu nchini Chad kimewashtua wananchi wa taifa hilo, na kimetokea baada ya kutangazwa mshindi wa uchaguzi wa urais uliofanyika wiki moja iliyopita.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kifo chake kimekuja, baada ya kuliongoza taifa hilo la Afrika ya Kati lenye utajiri wa mafuta kwa miaka 30 na tayari alikuwa amejihakikishia muhula wa sita kuendelea kuwa madarakani.
Deby ambaye alikuwa mwanajeshi ameuawa akiwa na umri wa miaka 68, na aliingia madarakani mwezi Disemba mwaka 1990 baada ya kuongoza vikosi vyake, wakati huo akiwa kiongozi wa waasi na kumwondoa madarakani kiongozi wa wakati huo Dikteta Hissene Habre aliyekimbilia nchini Senegal.
Baada ya kuongoza nchi hiyo kwa kipindi cha mpito kwa miaka sita, aliandaa Uchaguzi Mkuu na kuchaguliwa mwaka 1996 katika uchaguzi wa Kwanza wa vyama vingi.
Soma hapa pia-Rais wa Chad Idriss Deby auawa
Kuanzia mwaka 2001 alianza kupata shinikizo kutoka kwa wapinzani wake kwa kumshtumu kwa wizi wa kura na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu.
Mwaka 2005 aliandaa kura ya maoni na kuirekebisha katiba, na kufanikiwa kuondoa ukomo wa mihula kwa rais katika kipindi ambacho pia alishuhudia baadhi ya wanajeshi wakijaribu kumwondoa madarakani na waliposhindwa, walikimbilia karibu na mpaka wa Sudan na kuunda kundi la waasi.
Deby, amekuwa mshirika wa karibu sana na Ufaransa katika masuala ya usalama na mwaka 2012 alitoa kikosi cha wanajeji 2,000 kushirikiana na wale wa Ufaransa kupambana na wanajihadi Kaskazini mwa Mali, lakini pia jeshi la nchi yake limekuwa katika mstari wa mbele kupambana na magaidi wa Boko Haram.